Friday, January 18, 2013

BRANDTS AIONGOZA YANGA KATIKA MECHI YA 14 LEO


Brandts

KOCHA Mholanzi, Ernie Brandts leo anatarajiwa kuiongoza Yanga katika mechi ya 14 tangu ajiunge nayo Septemba mwaka huu, akitokea APR ya Rwanda wakati itakapomenyana na Black Leopard ya Afrika Kusini katika mchezo wa kirafiki, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
 
Yanga SC iliyorejea wiki Jumapili kutoka Uturuki kwenye kambi ya wiki mbili mjini Antalya, imekuwa ikijifua katika Uwanja wa Mabatini, Kijitonyama tangu Jumatano kwa ujumla kujiandaa na mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
Yanga leo itakutana na Black Leopard inayoshika nafasi ya 12 katika Ligi Kuu ya Afrika Kusini yenye timu 16, iliyowasili jana Dar es Salaam ikiwa na msafara wa watu 42 na kufikia katika hoteli ya White Sands, Mbezi Beach, Dar es Salaam.
Wachezaji wote walifanya mazoezi jana, kasoro kipa wa tatu, Yussuf Abdul na mshambuliaji Hamisi Kiiza 'Diego' wanaosumbuliwa na Malaria.
 
Katika mechi 13 ambazo Brandts ameiongoza Yanga hadi sasa tangu arithi mikoba ya Mbelgiji, Tom Saintfiet, ameshinda saba, kafungwa nne na kutoka sare mbili.
Kati ya hizo, mechi tisa ni za Ligi Kuu, ambazo amefungwa moja tu dhidi ya Kagera Sugar mjini Bukoba, wakati nyingine dhidi ya watani wa jadi, Simba SC alitoa sare ya 1-1 na saba ameshinda dhidi ya Toto African 3-1, Ruvu Shooting 3-2, Polisi Moro 3-0, JKT Oljoro 1-0, JKT Mgambo 3-0, Azam FC 2-0 na Coastal Union 2-0.
Nyingine zote za kirafiki kama ya leo, Yanga walifungwa 1-0 na Tusker Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kabla ya kwenda Uturuki, ambako walianza kwa sare ya 1-1 Ariminia Bielefed ya Daraja la Nne Ujerumani, kabla ya kufungwa 2-1 na Denizlispor FC ya Daraja la Kwanza Uturuki na 2-0 na Emmen FC ya Daraja la Kwanza Uholanzi.
REKODI YA ERNIE BRANDTS YANGA
Yanga 1-1 Simba SC            (Ligi Kuu)
Yanga 0-1 Kagera Sugar    (Ligi Kuu)
Yanga 3-1 Toto African      (Ligi Kuu)
Yanga 3-2 Ruvu Shooting  (Ligi Kuu)
Yanga 3-0 Polisi Moro       (Ligi Kuu)
Yanga 1-0 JKT Oljoro          (Ligi Kuu)
Yanga 3-0 JKT Mgambo     (Ligi Kuu)
Yanga 2-0 Azam FC             (Ligi Kuu)
Yanga 2-0 Coastal               (Ligi Kuu)
Yanga 0-1 Tusker                (Kirafiki)
Yanga 1-1 Ariminia Bielefed (Kirafiki)
Yanga SC 1-2 Denizlispor FC (Kirafiki)
Yanga SC 0-2 Emmen FC   (Kirafiki)
Yanga SC Vs Black Leopard (Kirafiki)

SOURCE bIN ZUBERY

No comments:

Post a Comment