Wednesday, August 1, 2012

Wakimbizi wa Burundi wavuliwa hadhi ya ukimbizi




Serikali, kuanzia leo tarehe 01 Agosti, 2012, imewavua hadhi ya ukimbizi wakimbizi 38,050 wa kutoka Burundi wanaohifadhiwa katika kambi  ya wakimbizi ya Mtabila iliyoko wilayani Kasulu mkoani Kigoma.Uamuzi huu wa kuwavua hadhi ya ukimbizi umefanywa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi kwa Mamlaka aliyopewa chini ya Kifungu cha 4 cha Sheria ya Wakimbizi.
 
 
Kufuatana na Sheria hiyo mkimbizi anapoteza hadhi ya ukimbizi kama mazingira yaliyomfanya kuwa mkimbizi yatakuwa hayapo tena, na atavuliwa hadhi hiyo kama ataendelea kukaidi maagizo halali ya kumtaka kurejea kwao kwa hiari.
 
 
 
Hatua ya kuwavua hadhi ya ukimbizi wakimbizi hawa imefikiwa baada ya Serikali za Tanzania na Burundi na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) kujiridhisha kuwa hapakuwa tena na sababu ya kuendelea  kuwahifadhi wakimbizi hao baada ya hali ya amani kurejea nchini mwao na hivyo kuwataka kurejea kwao.
 


 
Zoezi la kuwasaili wakimbizi waliopo katika kambi ya wakimbizi ya Mtabila lilifanyika kuanzia mwezi Septemba hadi Desemba mwaka 2011 kwa lengo la kubaini kama walikuwepo wakimbizi wenye sababu za msingi za kuendelea kuwepo nchini, ambapo ilibainika kuwa wakimbizi 38,050 hawakuwa na sababu za kuendelea kuwa wakimbizi.
 
 
Kufuatia matokeo ya zoezi hilo, Kikao cha Pande Tatu, kilichojumuisha wawakilishi wa Serikali  za Tanzania na Burundi na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), kilifanyika jijini Bujumbura nchini Burundi tarehe 22 Februari, 2012 na kukubaliana kwa pamoja kuifunga kambi ya Mtabila ifikapo tarehe 31 Desemba, 2012.
 
 
Baada ya kuwavua hadhi ya ukimbizi, raia hawa wa Burundi sasa wataendelea kusaidiwa kurejea kwao kwa hiari hadi tarehe 31 Desemba mwaka huu, ambapo Kambi hiyo ya Mtabila itafungwa rasmi, na wale ambao watakuwa hawajaondoka baada ya tarehe hiyo watachukuliwa kuwa ni wahamiaji haramu, na kushughulikiwa kufuatana na Sheria ya Uhamiaji.
 

Historia ya hifadhi ya wakimbizi hapa nchini ilianza tangu mwaka 1961 ambapo Tanzania ilikuwa na idadi kubwa ya wakimbizi kutoka nchi mbalimbali za Afrika, idadi ambayo katika miaka ya tisini ilifikia takribani milioni moja, 641,386 kati yao wakiwa ni wakimbizi kutoka Burundi.
 


Zoezi la kuwarejesha  kwao wakimbizi wa Burundi lilianza rasmi mwaka 2002 baada ya nchi yao kurejea katika hali ya amani na hadi sasa kambi nane zilizokuwa zikihifadhi wakimbizi toka Burundi zimefungwa. Kambi hizo ni Karago, Mtendeli, Kanembwa na Nduta zilizokuwa wilayani Kibondo, na Muyovosi iliyokuwa wilayani Kasulu, mkoani Kigoma.
 
 
Kambi nyingine zilizofungwa ni Kitali iliyokuwa wilayani Biharamulo, Lukole A na B zilizokuwa wilayani Ngara, mkoani Kigoma.Kambi ya wakimbizi ya Mtabila ndiyo itakuwa ya mwisho kufungwa katika mlolongo wa kambi zilizokuwa zikihifadhi wakimbizi kutoka Burundi hapa nchini.

source:mwanawamakonda.blogspot.com

Ngassa atua rasmi Simba



Mshambuliaji wa Taifa Stars Mrisho Ngassa amesajiliwa na wekundu wa msimbazi Simba kwa mkataba wa miaka miwili toka Klabu yake ya zamani Azam FC hivyo kumaliza uvumi kuwa alikuwa anajiandaa kutua Jangwani.

Azam wamefikia uwamuzi wa kumuuza Ngassa kwa kile walichokiita mapenzi ya dhati aliyonayo na klabu ya Yanga ya jijini Dar es salaam.

nitakuletea taarifa zaidi za habari hii

BAHANUZI,SURE BOY,REDONDO,CHUJI WAITWA KWENYE KIKOSI CHA TIMU YA TAIFA


Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen leo (Agosti 1 mwaka huu) ametangaza kikosi cha wachezaji 21 kwa ajili ya mechi ya kirafiki itakayochezwa ugenini Agosti 15 mwaka huu.
 
Wachezaji walioitwa Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager wanatakiwa kuripoti kambi kwenye hoteli ya Tansoma, Dar es Salaam, Agosti 8 mwaka huu saa 1 jioni tayari kwa mazoezi yatakayoanza siku inayofuata.
 
Makipa walioitwa kwenye kikosi hicho ni Deogratias Munishi (Azam), nahodha Juma Kaseja (Simba) na Mwadini Ali (Azam). Mabeki ni nahodha msaidizi Aggrey Morris (Azam), Erasto Nyoni (Azam), Kelvin Yondani (Yanga) na Shomari Kapombe (Simba).
 
Viungo ni Athuman Idd (Yanga), Frank Domayo (Yanga), Haruna Moshi (Simba), Mrisho Ngassa (Azam), Mwinyi Kazimoto (Simba), Ramadhan Chombo (Azam), Ramadhan Singano (Simba), Salum Abubakar (Azam) na Shabani Nditi (Mtibwa Sugar).
 
Wachezaji wanaounda safu ya ushambuliaji ni John Bocco (Azam), Mbwana Samata (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC), Said Bahanuzi (Yanga), Simon Msuva (Yanga) na Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC).

Source shaffih Dauda in sports.

HATIMAYE-LIGI KUU YA MSIMU UJAO KUENDESHWA NA KAMPUNI-TFF WAIPITISHA




KWA mara ya kwanza Ligi Kuu Bara itaandika historia msimu ujao, ambapo sasa itasimamiwa na kuendeshwa na kampuni, 'Tanzania Premium League' (TPL). Hatua ya kupitisha mabadiliko hayo, ilifikiwa katika kikao cha siku mbili cha Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Akizungumza jana, mwenyekiti wa kamati ya kuendesha mchakato wa kampuni, Wallace Karia alisema TFF imepitisha kampuni kuwa chombo huru cha kuendesha ligi hiyo itakayoanza rasmi Septemba Mosi mwaka huu.

"Tulichokuwa tunatofautiana na TFF juu ya ligi kuendeshwa na chombo huru, lakini sasa kamati ya utendaji imetoa baraka," alisema Karia."Kuna mambo madogo ya kufanyiwa mabadiliko, hata hivyo hali hiyo siyo kikwazo cha ligi kusimamiwa na chombo huru," aliongeza Kiria.

Karia alisema baadhi ya maeneo ya kufanyiwa marekebisho ni suala la muundo wa kisheria wa uendeshaji ligi na kasoro ndogo walizozibaini awali.

Kimuundo kutakuwa na Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi wa TPL, kiongozi wa juu wa klabu iliyoshinda Ligi Kuu msimu uliotangulia.

Pia kutakuwa na Makamu Wenyeviti wa Bodi watatu, ambao ni viongozi wa juu wa timu mbili zilizoshika nafasi ya pili na tatu na Makamu wa pili wa Rais wa TFF anayewakilisha klabu.

"Pia bodi ya wakurugenzi wa kampuni ya Ligi Kuu inahusisha wenyeviti au wakurugenzi au kiongozi wa juu wa klabu zote 14 (16) zinazocheza Ligi Kuu, ambapo kila klabu itatoa mjumbe mmoja na TFF pia itakuwa na hisa kwenye kampuni.

Wajumbe wengine wa bodi ya wakurugenzi wa kampuni ya ligi ambao hawatapiga kura ni mjumbe mmoja kutoka Chama cha Wanasoka wa Kulipwa, Chama cha Waamuzi (FRAT), Chama cha Makocha (TAFCA0 na Wadhamini wa Ligi Kuu.

"Kutakuwa na kamati huru ya nidhamu na rufaa ambayo itateuliwa na Bodi ya wakurugenzi ya TPL kila mwaka. Maamuzi ya kamati hii yatapaswa kutekelezwa na klabu zote zinazoshiriki Ligi Kuu lakini yanaweza kupigwa kwenye Kamati ya Nidhamu na Rufaa ya TFF," aliongeza Kiria.

Uhusiano kati ya TPL na TFF utaruhusu Makamu wa pili wa Rais TFF kuwa makamu wenyeviti wa bodi ya wakurugenzi wa TPL.

Aidha, uchaguzi wa makamu wa rais wa TFF utafanywa na Bodi ya Wakurugenzi wa TPL au UTAFOC na kiongozi huyo atapaswa kuwa ama kiongozi wa juu wa klabu ya Ligi Kuu au Ligi Daraja la Kwanza au mmoja wa wanahisa wa Klabu inayoshiriki Ligi Kuu au Daraja la Kwanza.

Kuhusiana na mapato ya milango ambayo kwa sasa TFF inachukua asilimia 10, TPL itapaswa kutoa asilimia ya hisa za TFF kutoka pato lake na klabu zitapaswa kutoa asilimia tano (5%) pato la milangoni.

Kuhusu kumiliki hisa za kampuni, klabu zote zinazocheza Ligi Kuu zitakuwa na hisa sawa kwenye kampuni, ambazo zitapatikana kutokana na klabu kuwa mwananchama, na iwapo iwapo itashuka daraja, hisa zake zitahamia kwa klabu iliyopanda daraja.

Wakati huohuo, klabu zote 14 zinazoshiriki Ligi Kuu zinatarajia kufanya kikao leo kwenye ukumbi wa JB Delmont, ambapo moja ya ajenda ni kujadili kwa kina suala la kampuni hiyo.Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Yanga, Mwesigwa Celestine alikiri kuwapo kwa mkutano huo leo.

Msemaji wa Shirikisho la soka nchini, TFF, Boniface Wambura hakukataa wala kukubali taarifa hizo zaidi ya kusema wakati kikao cha Kamati ya Utendaji kinakutana, yeye hakuwepo ofisini. 



Source: Mwananchi